Tuesday, August 21, 2012

MAKARANI WA SENSA MANISPAA YA IRINGA WATAKIWA KUZINGATIA WALIYOFUNDISHWA


 Mgeni rasmi mkuu wa Wilaya ya Iringa Dkt Leticia Warioba akisoma risala mbele ya makarani wa sensa waliofuzu mafunzo yao.
 Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa Bi Theresia Mahongo akisisitiza jambi kabla ya kumkaribiasha mgeni Rasmi.
 
 
 Makarani wa sensa wakimsikiliza mgeni rasmi.
 


Zaidi ya Makarani 260 watakaoshiriki zoezi la sensa ya watu na makazi Manispaa ya Iringa mjini wametakiwa kutenda kazi hiyo kwa moyo na uaminifu mkubwa kama mafunzo yanavyosema ili taarifa zinazohitajika na serikali kupitia zoezi hilo la sensa ziweze kufanikiwa.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya makarani wa sensa yaliyoendeshwa kwa muda wa wiki moja Katika Manispaa ya IringaMjini, Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt. Leticia Warioba amesema anaamini makarani hao walipatiwa mafunzo yao ipasavyo kama wakufunzi walivyowafundisha mafunzo hayo na kusema wao wanategemewa kwa kiasi kikubwa kufanikisha zoezi hilo ambapo serikali imedhamiria kukusanya takwimu ya watu na makazi ifikapo tarehe 26 August ikiwa ni moja ya vipaumbele vya taifa.

Ameongeza kuwa madhumuni makubwa ya mafunzo hayo yalikuwa ni kuwawezesha na makarani na wadadisi ili waweze kukusanya takwimu sahihi. Amesema endapo watakiuka mafunzo waliyopatiwa kutapelekea zoezi hilo kutofanikiwa hali ambayo haitegemewi na yeye pamoja na serikali kwa ujumla hivyo wanatakiwa kutambua dhamana waliyokabidhiwa ni kubwa hivyo ni azima waifanye kama inavyotakiwa.

Pia amewataka kupambana na changamoto zitakazojitokeza na kuhakikisha wanatoa taarifa mapema kwa wasimamizi wao mara moja pindi wanapokutana na changamoto ili ziweze kutatuliwa haraka na zoezi la sensa liendelee.

Amewataka viongozi wa dini, siasa na wananchi kutoa ushirikiano katika kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika zoezi hili la sensa. Nakuwaomba wananchi kutunza kumbukumbu zote za taarifa za maswali yatakayoulizwa kwa wale watu waliolala katika kaya zao usiku wa kuamkia tarehe 26 Augusti mwaka huu. Nakuwataka wale ambao wana wake wengi kwa maana ya mkuu wa kaya kutoa taarifa sahihi ili kufanikisha zoezi.

Dkt Warioba ameongeza kuwa shughuli hizo za sensa hazitaathiri shughuli zao za kiuchumi na kijamii isipokuwa makarani wa sensa zitawachukua siku zisizo zidi saba katika kutekeleza zoezi hili kuanzia tarehe 26 mpaka tarehe 2.

Kwa upande wao makarani hao wamesema wanashukuru kwa mafunzo waliyopatiwa na wameahidi kuekeleza jukumu la sensa lililopo mbele yao kwani wanatambua dhamana waliyokabidhiwa hivyo wamemuahidi mkuu wa wilaya kuwa watafanikisha zoezi hilo kama inavyotegemewa na serikali na kutoa wito kwa wananchi kujitokeza ili kuweza kufanikisha zoezi hilo.

Zoezi la sensa ya watu na makazi litatekelezwa nchi nzima kuanzia usiku wa 25/08/2012 kuamkia Agosti 26, mwaka huu hivyo wananchi wote wanaombwa kushiriki zoezi hilo kikamilifu




0 comments:

Post a Comment